AFISA MIPANGO AWASILISHA RASIMU YA BAJETI YA SHILINGI BILIONI 25.7 NEWALA DC.
imeandikwa na Afisa Habari Shabani Mkumba
Afisa Mipango wa Halmashauri ya Wilaya ya Newala, Bw. Sylvester Ngonyani, amewasilisha Rasimu ya Mpango na Bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027 yenye jumla ya Shilingi Bilioni 25.7 katika kikao maalum cha Baraza la Madiwani kilichofanyika Februari 11, 2026, katika ukumbi wa Halmashauri.
Akiwasilisha rasimu hiyo, Bw. Ngonyani alisema kati ya kiasi hicho, Shilingi Bilioni 13.7 zinatokana na Ruzuku ya Mishahara, Shilingi Bilioni 3.8 ni Mapato ya Ndani ya Halmashauri, Shilingi Bilioni 1.3 ni Mchango wa Jamii, na Shilingi Bilioni 6.8 ni Ruzuku kwa Miradi ya Maendeleo kutoka Serikali Kuu na Wadau wa Maendeleo.
Alieleza kuwa bajeti hiyo imelenga kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za jamii, kuimarisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo, na kukuza uchumi wa wananchi wa Wilaya ya Newala. Aidha, kwa mwaka wa fedha 2026/2027, mapato ya ndani yanatarajiwa kuongezeka kwa Shilingi Milioni 161.5, sawa na asilimia 4.2, kutoka Shilingi Bilioni 3.7 za mwaka 2025/2026 hadi Shilingi Bilioni 3.8.
Bw. Ngonyani alisema ongezeko hilo linatokana na juhudi za kuimarisha vyanzo vya mapato kama ushuru wa korosho ghafi, ada za biashara, kodi ya majengo, pamoja na mapato yanayotokana na hospitali na vituo vya afya.
Akihitimisha, Afisa Mipango huyo alisisitiza umuhimu wa kuongeza ufanisi katika ukusanyaji wa mapato, uwajibikaji wa watendaji, na matumizi sahihi ya fedha za umma ili kufanikisha utekelezaji wa bajeti na kuinua ustawi wa wananchi wa Wilaya ya Newala.
Kitangari,Newala
Anuani ya Posta: P.O. Box 16
Simu: +255232410251
Mobile:
Barua pepe: ded@newaladc.go.tz
Hakimiliki@2016 Halmashauri ya Wilaya ya Newala. Haki zote zimehifadhiwa